Msamiati wa Mapambo

Mapambo ni vitu vinavyovaliwa na watu ili kujirembesha; kuwafanya wavutie machoni pa watu wengine;

Mifano

  1. bangili:
    ni pambo la duara linalovaliwa mkononi na wanawake.
  2. herini:
    ni pambo linalovaliwa kwenye ndewe la sikio.
  3. hina:
    ni rangi nyekundunyekundu inayopakwa miguuni na mikononi mwa wanawake.
  4. kago:
    ushanga unaovaliwa kiunoni
  5. kanta:
    ni rangi nyeusi inayopakwa kwenye mvi (nywele nyeupe) ili nywele zionekana kama nyeusi, hasa na wale wasiopenda uzee.
  6. keekee:
    ni pambo linalovaliwa na wanawake mkononi kama kikuku au bangili.
  7. kigesi:
    bangili/kikuku kinachovaliwa na wanawake miguuni.
  8. kikuku:
    pambo la duara linalovaliwa mkononi au mguuni.
  9. kipini:
    pambo linalovaliwa puani (sehemu ya juu)
  10. kishaufu:
    hili ni pambo la duara linalovaliwa puani (sehemu ya chini).
  11. mafuta:
    ni kitu kioevu kinachopakwa mwilini kwa makusudi ya kulainisha ngozi na kunukia vizuri.
  12. marashi:
    haya ni kifurushi, maji au mafuta yanayonukia vizuri yanayoundwa kwa mawaridi na kemikali nyingine yanayopakwa mwilini hasahasa kwapani.
  13. mkufu:
    ni kitu chembamba kama mnyororo kinachoundwa kwa madini kama dhahabu, fedha n.k kinachovaliwa shingoni.
  14. mshipi:
    ni mkanda unaovaliwa kiunoni.
  15. ndewe:
    ni tundu linalotobolewa kwenye sehemu ya chini ya sikio ili kuvaliwa mapambo ya sikioni.
  16. ndonya:
    ni tundu linalotobolewa katika sikio na mdomo wa juu au mdomo wa chini
  17. nembo:
    ni chale zinazochanjwa usoni au kwenye sehemu nyingine za mwili. Nembo zilitumika kuonyesha kubaleghe(kuvunja ungo) kwa wasichana; kubainisha kabila au kuonyesha urembo tu.
  18. njuga:
    kengele ndogondogo zinazovaliwa shingoni, miguuni na mikononi hasa wakati wa kucheza ngoma za kitamaduni.
  19. nti:
    ni vijiti vidogo vinavyovaliwa na wanawake masikioni baada ya kutoga ndewe.
  20. nyerere:
    ni uzi mwembamba wa madini unaovaliwa mikononi na miguuni.
  21. nywele bandia:
    ni nywele za kununua zinazovaliwa na kina dada ili kujiongezea urembo.
  22. pete:
    pambo la madini la duara linalovaliwa kidoleni.
  23. poda:
    ni rangi nyeupe, laini itumiwayo na wanawake kujipaka.
  24. rangi ya kucha:
    ni rangi inayopakwa kwenye kucha na wasichana
  25. rangi ya midomo:
    ni rangi nyekundunyekundu inayopakwa kwenye midomo na wanawake.
  26. saa:
    kifaa cha kupimia wakati kinachovaliwa mkononi kama pambo.
  27. tai:
    nguo/kitambaa kilichoundwa ili kuvaliwa shingoni juu ya shati haswa wakati wa shughuli rasmi
  28. taji:
    kofia inayovaliwa na wafalme, watawala au washindi kuashiria cheo chao au ushindi wao.
  29. ukaya:
    nguo au kitambaa kinachovaliwa kukinga sehemu ya mdomo hasa na wanawake Waislamu.
  30. usinga:
    nywele za farasi au nyumbu zinazovaliwa mkononi bangili.
  31. wanja:
    ni rangi nyeusi ya majimaji au ungaunga inayotumika na wanawake kupaka machoni, usoni, mikononi na hata miguuni.