Fasihi
Fasihi ni sanaa ya lugha. Fasihi hutumia lugha kutoa sanaa mbalimbali katika jamii.
Tanzu za Fasihi
Kuna tanzu mbili kuu za fasihi, na kila utanzu una vipera vyake: Fasihi Simulizi na Fasihi Andishi:
Fasihi Simulizi
- Hadithi (Ngano) - hekaya, mighani, visasili n.k
- Nyimbo - za jandoni, za ndoa, za kazi n.k
- Maigizo - michezo ya kuigiza, ngomezi n.k
- Tungo Fupi - methali, vitendawili n.k
Fasihi Andishi
- Hadithi Fupi - hadithi isiyokuwa ndefu iliyochapishwa katika mkusanyiko wa hadithi nyingine
- Riwaya - hadithi ndefu iliyochapishwa katika kitabu chake pekee
- Tamthilia - mchezo wa kuigiza uliowekwa kwa maandishi
- Ushairi* - mashairi yaliyoandikwa
Tofauti kuu kati ya fasihi simulizi na fasihi andishi ni kwamba Fasihi Simulizi huwasilishwa kwa njia ya mdomo au matendo ilhali
Fasihi Andishi huwasilishwa kwa njia ya maandishi.
Tanbihi:Ushairi ni kipera cha nyimbo lakini pia mashairi yanaweza kuwa chini ya Fasihi Andishi, ikiwa yamechapishwa.
Tofauti kati ya Fasihi Andishi na Fasihi Simulizi
FASIHI SIMULIZI | FASIHI ANDISHI | |
1. | Huwasilishwa kwa njia ya mdomo na/au matendo. | Huwasilishwa kwa njia ya maandishi |
2. | Ni mali ya jamii. | Kazi andishi ni mali ya mwandishi (na mchapishaji) |
3. | Msimulizi anaweza kubadilisha sehemu fulani | Kitabu kilichoandikwa hakiwezi kubadilishwa |
4. | Huhifadhiwa akilini | Huhifadhiwa vitabuni |
5. | Kazi simulizi hubadilika na wakati | Kazi andishi haibadiliki na wakati |
6. | Huhitaji msimulizi na hadhira yake wawe mahali pamoja wakati wa masimulizi | Msomaji anaweza kusoma kitabu cha hadithi peke yake, mahali popote, wakati wowote |
7. | Mtu yeyote anaweza kutunga na kusimulia | Ni lazima mwandishi na msomaji wawe na uwezo wa kusoma |
8. | Hutumia wahusika changamano (wanyama, watu, mazimwi n.k) | Hutumia wahusika wanadamu. |
Umuhimu wa Fasihi Katika Jamii
- Kuburudisha jamii. Takribani vipera vyote vya fasihi huwa na kusudi la kufurahisha, kutumbuiza na kusisimua hadhira.
- Kuelimisha. Fasihi hukusudia kuelimisha hadhira kuhusu jamii, mazingira n.k
- Kudumisha maadili katika jamii kwa kuelekeza, kuonya na kunasihi hadhira jinsi ya kufuata mwelekeo unaokubalika katika jamii.
- Kuunganisha jamii. Fasihi huleta pamoja watu katika jamii. Kwa mfano, katika nyimbo, miviga, vichekesho.
- Kukuza lugha. Aghalabu tungo zote za fasihi hutumia lugha. Isitoshe, fasihi hutumia mbinu nyingi za lugha. Wasimulizi na waandishi wa fasihi huhitaji kuwa na ukwasi wa lugha.
- Kuhifadhi mila, tamaduni na itikadi za jamii. Aghalabu kazi za fasihi (hasahasa Fasihi Simulizi) huambatanishwa na desturi mbalimbali za jamii husika.
- Kukuza uwezo wa kufikiri. Vipera vingi vya fasihi huwachochea hadhira kufikiri sana ili kupata suluhisho. k.m vitendawili, ngano za mtanziko n.k